SHURA YA MAIMAMU ARUSHA YATOA TAMKO ZITO MACHAFUKO YA UCHAGUZI,YATAKA TUME HURU YA UCHUNGUZI KUTENDA HAKI ILI KUPATA MWAROBAINI,WAKOSOA MATAMKO YA TEC

 Na Joseph Ngilisho, ARUSHA

Viongozi Shura ya Maimamu -Arusha

SHURA ya Maimamu na Viongozi wa Taasisi za Kiislamu  Arusha ,imetoa tamko kali la kulaani machafuko ya uchaguzi wa Oktoba 29, mwaka huu, na kutaka hatua madhubuti zichukuliwe kurejesha na kulinda amani ya nchi.

Katika mkutano na waandishi wa habari uliofanyika jijini Arusha, Mlezi wa Shura hiyo, Sheikh Juma Ikusi, alisema machafuko yaliyotokea yameacha majeraha na kuchafua taswira ya taifa lililojengwa kwa misingi ya umoja na mshikamano tangu enzi za waasisi.
Sheikh Juma Ikusi -Mlezi Shura ya Maimamu Arusha.

Sheikh Ikusi alisisitiza kuwa Tume Huru ya Uchunguzi iliyoundwa na Rais Samia Suluhu Hassan inapaswa kuja na majibu ya kweli, ya kina na yatakayoponya majeraha yaliyosababishwa na tukio hilo, ili kuepusha kurudiwa kwa machafuko nchini.

Alitaka tume hiyo iwe shirikishi kwa kujumuisha makundi yote muhimu katika jamii—taasisi za dini, vyama vya siasa, wadau wa maendeleo, asasi za kiraia, mashirika ya haki za binadamu, chama cha wanasheria pamoja na makundi maalumu.

Akiendelea kusoma tamko hilo, Sheikh Ikusi aliwataka Waislamu wote nchini kutojihusisha na maandamano yanayodaiwa kutarajiwa kufanyika Desemba 9, akisema maandamano hayapo katika misingi ya kujenga amani na yanaweza kuongeza mpasuko.

Katika tamko hilo, Sheikh Ikusi alionyesha kukerwa na baadhi ya matamko yaliyotolewa na viongozi wa Kikristo kupitia Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania (TEC), akidai kuwa yaliweza kuchochea mazingira ya vurugu wakati wa uchaguzi.

Hata hivyo, alisisitiza kuwa mafundisho ya kweli ya dini zote, ikiwemo Ukristo, yanaweka amani mbele ya mambo yote. Alinukuu maandiko yanayoonesha kuwa hata Yesu alipokutana na watu, aliwasalimu kwa kauli ya kuhimiza utulivu na upendo, akisema:
“Amani iwe nanyi,” ikiwa ni ishara ya kuonyesha thamani ya amani katika mafundisho ya dini zote.

Shura ya Maimamu ilisisitiza kuunga mkono hatua ya Rais Samia ya kuunda Tume Huru ya Uchunguzi, wakisema ni hatua sahihi ya kupata ukweli, kujenga maridhiano na kurejesha mshikamano wa taifa.

Yataka uchunguzi wa kina kwenye chanzo cha machafuko

Tamko hilo limeitaka tume hiyo kuchunguza masuala muhimu, ikiwemo,Nani au kikundi gani kilichochochea machafuko na kusababisha uharibifu wa mali na vifo.Mapungufu ya serikali au mifumo ya usimamizi wa uchaguzi.

Sababu za vijana kujihusisha na vurugu, ikiwemo ukosefu wa ajira au vishawishi vya watu wanaotaka kuivuruga nchi.Hatua za kuwajengea vijana matumaini na kuwaepusha na mihemko hatarishi.

Shura hiyo imependekeza tume hiyo ihakikishe inashirikisha makundi yote ya kijamii—taasisi za dini, asasi za kiraia, vyama vya siasa, mashirika ya haki za binadamu pamoja na makundi maalumu—ili kupata majibu ya kweli na yanayokubalika na pande zote.

Sheikh Ikusi aliitahadharisha jamii dhidi ya kauli za uchochezi zinazosambaa mtandaoni zinazodaiwa kutolewa na watu wanaojiita Waislamu, akisema hizo si fundisho la dini na zinapaswa kupuuzwa.

> “Tusipowakemea watu hawa, taifa letu linaweza kuingia katika hali ya machafuko kama baadhi ya nchi jirani ambako vurugu zimekuwa zikijirudia bila kikomo,” alisema.


Shura ya Maimamu imeunga mkono matamko ya BAKWATA, Umoja wa Wanazuoni wa Kiislamu Tanzania, pamoja na hotuba ya Rais Samia aliyoitoa wakati wa uzinduzi wa Bunge.

Viongozi wa dini waliohudhuria tamko hilo, akiwemo Sheikh Suleiman Mgulumah na Sheikh Farajallah Soly, waliwahimiza Watanzania kuendelea kuilinda amani, wakiitaja kuwa ndiyo msingi wa maendeleo na ustawi wa taifa.







Ends

Post a Comment

0 Comments