SIMULIZI YA MACHUNGU YA SABINA JOHN MOSI: Kutoka Maisha ya Mafanikio Hadi Kuishi Kwa Kutangatanga Baada ya Mgogoro wa Ndoa
Na Mwandishi Wetu | Arusha
SIMULIZI YA MAOMBI, MATUMAINI NA MAONO YA MAISHA
Na Mwandishi Wetu
Katika simulizi yenye kugusa hisia za wengi, SABINA JOHN MOSI ameibuka hadharani kueleza changamoto nzito anazopitia huku akiwaomba viongozi wa serikali, vyombo vya sheria, wadau wa usalama pamoja na jamii kwa ujumla kutekeleza ahadi walizompa za kumsaidia katika kipindi kigumu anachopitia.
Ameanza kwa kutoa shukrani kwa wote waliomuahidi msaada na kuridhia kusimama naye katika changamoto hizo, akiwemo Waziri Mkuu, Waziri wa Michezo, Mkuu wa Wilaya ya Arumeru, Diwani, Afisa Tarafa, Mtendaji, Mwenyekiti pamoja na Mabalozi wa eneo analoishi.
Aidha, amewashukuru baadhi ya viongozi wa Jeshi la Polisi kutoka Makao Makuu, akiwemo R.C.O, Deputy OCCD, OCD pamoja na baadhi ya askari polisi wa Arusha aliowataja kuwa wameonyesha moyo wa utu na msaada katika kipindi kigumu anachopitia.
Pia amesema baadhi ya wanajeshi wema akiwemo Captain na Major aliowaomba msaada wa ulinzi na usalama wake pamoja na watu wake na mali zao walikubali kumsaidia.
Katika upande wa msaada wa kisheria, amesema amewafikia wadau mbalimbali wakiwemo Tanganyika Law Society, taasisi za haki za binadamu pamoja na Mama Samia Legal Aid ambao walikubali kumpatia msaada wa kisheria. Vilevile amewashukuru waandishi wa habari kwa umoja wao pamoja na mabouncers na bodyguards kwa mshikamano wao.
Amesema jamii yenye upendo na huruma nayo imeahidi kushirikiana naye katika kutatua changamoto mbalimbali zinazomkabili kwa sasa.
Miongoni mwa mambo anayoyaomba kusaidiwa ni pamoja na hukumu zilizokwisha kutolewa zipitiwe kwa kina, kesi zilizopo mahakamani tangu mwaka 2021 zimalizike mapema, pamoja na kupatiwa sehemu ya kuishi baada ya kudai kunyang’anywa nyumba zote alizokuwa akimiliki.
Aidha ameomba watoto wengi aliokuwa akiishi nao kama mlezi wasaidiwe mahitaji muhimu baada ya baadhi yao kuishi mitaani kufuatia hali hiyo.
Katika upande wa kifamilia, ameomba apewe talaka kisheria na kwa wakati bila pingamizi, huku akisisitiza kuwa mtoto wake mdogo asisome shule ya boarding ili aweze kumpa huduma za kiroho na kimwili pamoja na kumfundisha sheria na wajibu.
Kadhalika ameomba msaada wa ada na mahitaji kwa mtoto anayesoma sekondari pamoja na anayesoma chuo ambaye hana mkopo wa elimu ya juu.
Kwa upande wa mali, ameomba magari yake 11 aina ya Scania (8), Vanguard, IST na Suzuki yarejeshwe, huku akiomba magari mawili aina ya Nissan Hilux na Ipsum yaliyokabidhiwa kwenye mirathi yaendelee kuwa salama.
Amedai pia kuwa kuna zaidi ya shilingi bilioni mbili zilizopo katika benki tofauti ambazo ameomba zibaki salama hadi kesi zinazomkabili zitakapomalizika.
Sambamba na hilo ameomba nyumba tano zitembelewe na kuwekewa zuio zikiwemo zilizopo maeneo ya Lawate, Kibosho, Sakina, Ngarenaro na Kona Nairobi.
Vilevile ameomba kusaidiwa kurejeshewa nyaraka za nyumba na magari baada ya kumaliza kulipa mkopo unaodaiwa kufikia zaidi ya shilingi milioni 370.
Katika changamoto nyingine, ameomba apewe muda wa kulipa deni la shilingi milioni mbili bila kifungo kinachomkabili kwa sasa.
Pia ameomba msaada wa huruma na msaada wa kisheria kwa rafiki zake Antony Gordon’s pamoja na Christian Khalid waliodaiwa kudhulumiwa zaidi ya shilingi milioni 500 hapa nchini. Ameeleza kuwa wawili hao ni raia wa Jamaica wanaoishi London nchini England na kusaidiwa kwao kutasaidia kuondoa hofu kwa wawekezaji wa kigeni kuhusu hali ya haki nchini.
Licha ya changamoto hizo, amesema bado ana matumaini ya kusimama tena maishani. Ameeleza kuwa amepitia maradhi, kuvamiwa, kuibiwa, kujeruhiwa mara kwa mara, majaribio ya kufungwa na hata kutolewa uhai pasipo sababu, pamoja na kutengwa na mwenzi na baadhi ya marafiki.
Hata hivyo amesema bado anaamini katika Mungu na maandiko matakatifu yanayohimiza kutokata tamaa, kuwa jasiri na kuwa na moyo wa ushujaa.
Akiendelea kusimulia maisha yake, SABINA amesema katika harakati zake za kutafuta riziki kama msambazaji wa mazao, vipodozi, bidhaa za chakula, magari na bidhaa mbalimbali ndani na nje ya nchi, aliwahi pia kutoa huduma kwa jamii kama mwalimu na mshauri kwa watu waliokuwa wakipitia nyakati ngumu.
Katika safari hiyo amesema alikumbana na mambo mengi mabaya yakiwemo ufisadi, uvamizi, wizi, unyonyaji, ulevi, uvivu, uzembe, ujinga, ubinafsi na uoga hali iliyomfanya kuanza kufikiria miradi na huduma alizozipa jina la “Nuru” na “Melita Hope”.
Amesema kabla ya kuanza mipango hiyo alimwomba Mungu kumpa kibali, hekima, maarifa, busara, ufahamu, nguvu na uwezo ili aweze kutimiza malengo yake.
Aidha amesema alipata nafasi ya kusoma elimu ya theolojia ili kutambua mema na mabaya, sambamba na kujifunza kuhusu rasilimali za nchi. Alisema alitamani kufahamu ni nani hasa wanaonufaika na rasilimali hizo ndipo akaanza kujifunza elimu ya miamba na madini (Geology) pamoja na baadhi ya lugha za kimataifa.
Ameeleza kuwa bado alikuwa na ndoto ya kusoma sheria, urubani na taaluma nyingine nyingi akiamini kuwa elimu haina mwisho na ndiyo ufunguo wa maisha.
Katika maono yake ya baadaye amesema baada ya kupata haki zake pamoja na kurejeshewa fedha na mali zake, atashirikiana na viongozi wa dini, viongozi wa serikali, wananchi na wageni wenye nia njema kuleta usawa, haki, mabadiliko mema, amani, furaha na matumaini kwa jamii.
Amefafanua kuwa kupitia mshikamano huo, watatoa huduma kwa wahitaji ikiwemo chakula, mavazi, makazi, afya, elimu, ulinzi, misaada ya kisheria pamoja na mikopo.
Pia amesema watatoa kipaumbele kwa miundombinu kwa kujenga barabara, kusambaza umeme wa jua na kuchimba visima huku wakiwafikia watu waliopo mitaani, vijijini, mashuleni, vyuoni, magerezani na vituo vya kulelea wasiojiweza.
Katika maono hayo pia amesema wanatarajia kuwekeza katika sekta mbalimbali zikiwemo madini, utalii, nishati, ukandarasi, usafiri wa anga, maji na nchi kavu, uvuvi, kilimo na ufugaji ili rasilimali hizo ziwanufaishe wananchi wote na dunia kwa ujumla.
Aidha amesema wana ndoto ya kuwa na viwanda vingi nchini vitakavyozalisha bidhaa zenye ubora wa hali ya juu huku vijana wakipata ajira zenye mishahara mizuri pamoja na kufundishwa kujiajiri.
Kwa mujibu wake,SABINA anaamini Tanzania inaweza kuwa miongoni mwa nchi tajiri duniani ikiwa itaweka mbele haki, usawa, elimu na matumizi sahihi ya rasilimali zake.
Akihitimisha simulizi yake, ameomba wazazi, mjomba wake, madaktari wake, mwanasheria wake, auditor, accountant, mameneja, viongozi wa TRA pamoja na jamii kwa ujumla kushirikishwa ili waweze kujadili na kufuatilia suala hilo kwa upana zaidi.
Ends..

0 Comments