Breaking🔥

KIKONGWE WA MIAKA 101 AKAMATWA AKIUZA BANGI

KIKONGWE WA MIAKA 101 AKAMATWA AKIUZA BANGI

Na Joseph Ngilisho | Arushadigital

MWANAMKE anayekadiriwa kuwa na umri wa miaka 101, Esther Ogunmabo, amekamatwa nchini Nigeria kwa tuhuma za kujihusisha na biashara haramu ya bangi, tukio lililoibua gumzo katika mitandao ya kijamii na vyombo vya habari nchini humo.

Ogunmabo alikamatwa Jumamosi katika Jimbo la Ogun, Kusini-Magharibi mwa Nigeria, wakati maofisa wa Shirika la Kitaifa la Kudhibiti Dawa za Kulevya (NDLEA) walipokuwa wakifanya operesheni dhidi ya biashara haramu ya dawa za kulevya.

Kwa mujibu wa NDLEA, mwanamke huyo mwenye umri wa zaidi ya karne moja alikutwa na vifurushi vya bangi aina ya skunk vilivyokuwa vimeandaliwa kwa ajili ya kuuzwa rejareja.

Mkurugenzi wa Mawasiliano wa NDLEA, Femi Babafemi, alisema vifurushi hivyo vilikuwa na jumla ya gramu 90 za bangi, ambazo mtuhumiwa alidai alikuwa akiwauzia wakazi wa eneo hilo.

Babafemi alisema wakati wa mahojiano, Ogunmabo aliwaeleza wachunguzi kuwa alianza kujihusisha na biashara hiyo baada ya duka lake kuteketea kwa moto, hali iliyomweka katika mazingira magumu ya kiuchumi.

Kukamatwa kwa mwanamke huyo mwenye umri wa zaidi ya miaka 100 kumezua mijadala nchini Nigeria, huku wengi wakishangazwa na madai ya kuhusika kwake katika biashara ya dawa za kulevya licha ya umri wake mkubwa.

NDLEA inaendelea na uchunguzi wa tukio hilo, huku hatua zaidi za kisheria zikitarajiwa kuchukuliwa dhidi ya mtuhumiwa kwa mujibu wa sheria za Nigeria.

Post a Comment

Previous Post Next Post