Breaking🔥

LUKUMAY AKAGUA UJENZI WA SHULE YA MANYIRE YA SH584 MILIONI

 LUKUMAY AKAGUA UJENZI WA SHULE YA MANYIRE YA SH584 MILIONI

Na Joseph Ngilisho | ARUMERU

MBUNGE wa Arumeru Magharibi, Dkt. Johannes Lembulung Lukumay, amekagua maendeleo ya ujenzi wa Shule mpya ya Sekondari Manyire wenye thamani ya Sh584 milioni, mradi unaolenga kupunguza msongamano wa wanafunzi katika Shule ya Sekondari Mlangarini na kuwasaidia wanafunzi wa Manyire kupata elimu karibu na makazi yao.


Taarifa hiyo imetolewa na Mkuu wa Shule ya Sekondari Manyire, Mwalimu Leshai Moita, wakati akisoma risala ya shule hiyo mbele ya Mbunge Lukumay katika ziara yake ya kukagua maendeleo ya ujenzi wa mradi huo.

Moita alisema mradi huo, unaogharimu Sh584 milioni, unahusisha ujenzi wa madarasa nane, mabweni manne, vyoo vya wasichana na wavulana vyenye jumla ya matundu nane, jengo la utawala pamoja na maktaba.

Alisema ujenzi wa shule hiyo utasaidia kupunguza changamoto ya wanafunzi wa Manyire kutembea umbali mrefu kwenda Shule ya Sekondari Mlangarini, sambamba na kupunguza msongamano wa wanafunzi katika shule hiyo.

“Lengo la mradi huu ni kujenga shule mpya ya Sekondari Manyire ili kupunguza msongamano wa wanafunzi katika Sekondari ya Mlangarini na kuwapa wanafunzi wanaotoka Manyire fursa ya kupata elimu karibu na maeneo yao,” alisema Moita.

Alisema mradi huo ulitambulishwa kwa wananchi Juni 4, 2026 na timu ya wataalamu kutoka Halmashauri, chini ya usimamizi wa Afisa Elimu Sekondari, kabla ya taratibu nyingine za utekelezaji kuendelea.

Kwa mujibu wa Moita, utekelezaji wa mradi ulianza rasmi Julai 2, 2026, ambapo wananchi wa Manyire walijitokeza kushiriki katika uchimbaji wa misingi ya miundombinu iliyokuwa tayari imepimwa na mkandarasi na kuainishwa katika BOQ.

SH247.5 MILIONI ZATUMIKA

Moita alisema hadi sasa Sh247.5 milioni zimetumika katika utekelezaji wa mradi huo, huku kiasi cha Sh336.7 milioni kikiwa bado hakijatumika.

Alisema ushiriki wa wananchi katika ujenzi huo unaonyesha umuhimu wa ushirikiano kati ya Serikali na jamii katika kutekeleza miradi yenye manufaa kwa wananchi.

Mradi huo unatarajiwa kuwa na mchango mkubwa katika kuboresha mazingira ya elimu kwa wanafunzi wa Manyire na maeneo ya jirani, huku pia ukisaidia kupunguza mzigo wa wanafunzi katika Shule ya Sekondari Mlangarini.

Katika ziara hiyo, Mbunge Lukumay alipata fursa ya kukagua hatua zilizofikiwa katika ujenzi na kupokea taarifa ya utekelezaji wa mradi kutoka kwa uongozi wa shule.



Ends

Post a Comment

أحدث أقدم