LISSU AFIKISHWA MAHAKAMA KUU KESI YA KIKATIBA IKISIKILIZWA
Na Arushadigital| DODOMA
Mwenyekiti wa CHADEMA, Tundu Lissu, leo Julai 20, 2026 amefikishwa katika Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Kuu ya Dodoma, kwa ajili ya kusikilizwa kwa shauri la kikatiba linalohusu haki ya mawakili kukutana na kuzungumza kwa faragha na wateja wao waliopo gerezani.
Shauri hilo limefunguliwa na mawakili wake, Kulwa William Maduhu, Nashon Nkung na Paul Kisabo, wakipinga utaratibu unaodaiwa kutumiwa na Mamlaka ya Gereza la Ukonga jijini Dar es Salaam wa kutowaruhusu kuzungumza kwa faragha na mteja wao wanapomtembelea gerezani.
Kwa mujibu wa walalamikaji, hatua hiyo inakiuka haki za kikatiba za mteja wao pamoja na haki ya mawakili kutekeleza wajibu wao wa kisheria bila kuingiliwa, hivyo kuiomba Mahakama Kuu kutoa tafsiri na maelekezo kuhusu uhalali wa utaratibu huo.
Kesi hiyo inasikilizwa na jopo la majaji watatu wa Mahakama Kuu linaloundwa na Jaji Amir Mruma, Jaji Dkt. Angelo Rumisha na Jaji Dkt. Evaristo Longopa, huku usikilizwaji wake ukifanyika kupitia Masjala Ndogo ya Dar es Salaam.
Lissu anaendelea kushikiliwa gerezani tangu Julai 10, 2025, akikabiliwa na kesi ya uhaini inayosikilizwa katika Mahakama Kuu ya Tanzania.
Shauri la kikatiba linatarajiwa kutoa mwongozo kuhusu haki za mawakili kupata faragha wanapokutana na wateja wao waliopo mahabusu au gerezani, suala ambalo limekuwa likizua mjadala miongoni mwa wadau wa sheria na haki za binadamu.
Ends..

Post a Comment