SAMIA AFANYA UTEUZI, UHAMISHO WA VIONGOZI SABA SERIKALINI
Na Arushadigital
RAIS wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, amefanya uteuzi na uhamisho wa viongozi saba katika Utumishi wa Umma, hatua inayolenga kuimarisha ufanisi wa utendaji katika wizara na taasisi mbalimbali za Serikali.
Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa leo Julai 22, 2026 na Katibu Mkuu Kiongozi, Balozi Dkt. Moses Kusiluka, miongoni mwa walioteuliwa ni Dkt. Latifa Mohammed Khamis, ambaye amekuwa Naibu Katibu Mkuu katika Ofisi ya Makamu wa Rais anayeshughulikia masuala ya Muungano.
Pia, Bi. Prisca Burton Lwangili ameteuliwa kuwa Naibu Katibu Mkuu katika Ofisi ya Rais – Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora.
Katika mabadiliko hayo, Abdallah Hassan Mitawi amehamishwa kutoka Ofisi ya Makamu wa Rais na kwenda kuwa Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Uchukuzi, huku Balozi Baraka Haran Luvanda akihamishiwa Wizara ya Katiba na Sheria katika nafasi hiyo hiyo.
Kadhalika, Dkt. Franklin Jasson Rwezimula amehamishwa kutoka Wizara ya Katiba na Sheria kwenda kuwa Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi, wakati Dkt. Maduhu Isaac Kazi amehamishwa kutoka Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi na kwenda kuwa Naibu Katibu Mkuu katika Ofisi ya Makamu wa Rais anayeshughulikia masuala ya Mazingira.
Mbali na uteuzi huo, Rais Samia amemteua Ephraim Balozi Mafuru kuwa Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Maendeleo ya Biashara Tanzania (TANTRADE), akitokea Bodi ya Utalii Tanzania (TTB), ambako alikuwa akihudumu kama Mkurugenzi Mkuu.
Taarifa ya Katibu Mkuu Kiongozi imeeleza kuwa uapisho wa Naibu Makatibu Wakuu walioteuliwa utafanyika katika tarehe itakayopangwa baadaye.

Post a Comment