WIZARA YA AFYA NA TAMISEMI ZABAINISHA MIKAKATI YA KUIMARISHA HUDUMA ZA AFYA NCHINI
Na Joseph Ngilisho – Dodoma
Wizara ya Afya kwa kushirikiana na Ofisi ya Waziri Mkuu – TAMISEMI zimeainisha mikakati mahsusi ya kuimarisha utoaji wa huduma za afya kuanzia ngazi ya msingi hadi rufaa, ikiwa ni sehemu ya utekelezaji wa dira ya Serikali ya Samia Suluhu Hassan ya kuboresha sekta ya afya nchini.
Mikakati hiyo imebainishwa katika kikao cha pamoja kati ya Wizara hizo na Kamati za Kudumu za Bunge za Afya na Masuala ya UKIMWI pamoja na TAMISEMI, kilichofanyika Februari 13, 2026 katika Bunge jijini Dodoma.
Akizungumza katika kikao hicho, Naibu Waziri wa Afya, Florence Samizi, amesema Serikali imeendelea kuwekeza kwa kiwango kikubwa katika kuboresha huduma za afya ili kuhakikisha wananchi wanapata huduma bora, salama na kwa wakati.
Ameeleza kuwa maboresho hayo yanajumuisha ujenzi na ukarabati wa miundombinu ya kutolea huduma, ununuzi wa vifaa na vifaa tiba vya kisasa, pamoja na kuimarisha upatikanaji wa dawa katika ngazi zote—zahanati, vituo vya afya na hospitali za rufaa za kanda na kitaifa.
Kwa upande wake, Naibu Waziri, Ofisi ya Waziri Mkuu – TAMISEMI, Rajab Seif, amesema Serikali itaendelea kuimarisha usimamizi na uratibu wa huduma za afya katika mamlaka za serikali za mitaa ili kuhakikisha huduma zinawafikia wananchi kwa ubora uliokusudiwa.
Naye Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Afya na Masuala ya UKIMWI, Johannes Lukumay, ameipongeza Serikali kwa hatua zilizopigwa katika kusogeza huduma za afya karibu na wananchi, akieleza kuridhishwa na uwepo wa miundombinu, dawa na vifaa tiba katika maeneo ya msingi.
Ameitaka Wizara ya Afya na TAMISEMI kuendelea kushirikiana kwa karibu ili kuimarisha zaidi huduma za afya, hatua itakayosaidia taifa kufikia malengo ya muda mrefu ya kuboresha afya za Watanzania kuelekea mwaka 2050.
....Ends..

0 Comments