CHADEMA PEMBA YAMFUKUZA UANACHAMA SAID ISSA MOHAMMED
Na Arushadigital | Pemba
Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) Kanda ya Pemba kimetangaza kumvua uanachama mwanachama wake, Said Issa Mohammed, baada ya kupatikana na tuhuma za ukiukwaji wa nidhamu ya chama.
Uamuzi huo umefikiwa katika kikao cha dharura cha Kamati Tendaji ya Kanda ya Pemba kilichofanyika Juni 6, 2026 katika Ukumbi wa Pride ya Zamani, Chake Chake, Pemba, chini ya uongozi wa Mwenyekiti wa Kanda hiyo, Omar Nassor.
Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na CHADEMA Kanda ya Pemba, kikao hicho kilijadili kwa kina mwenendo wa Said Issa Mohammed kwa kuzingatia masharti ya Katiba, Kanuni na taratibu za chama kabla ya kufikia uamuzi wa kumfukuza uanachama.
Taarifa hiyo imeeleza kuwa kuanzia sasa Said Issa Mohammed hatambuliki tena kama mwanachama, kiongozi wala mwakilishi wa CHADEMA katika ngazi yoyote ya uongozi au shughuli za chama.
Aidha, chama hicho kimesisitiza kuwa kauli, matamshi au vitendo vyovyote vitakavyofanywa na Said Issa Mohammed baada ya hatua hiyo vitakuwa ni vya binafsi na havitahusishwa kwa namna yoyote na CHADEMA.
Hatua hiyo inaongeza sura mpya katika siasa za visiwani Pemba huku chama hicho kikisisitiza msimamo wake wa kuzingatia nidhamu, Katiba na taratibu za ndani katika uendeshaji wa shughuli zake za kisiasa.
Ends

Post a Comment