CCM YAPUUZA MAAGIZO YA MSAJILI KUJIELEZA KUHUSU KAULI TATA YA MARY CHATANDA?

 CCM YAPUUZA MAAGIZO YA MSAJILI KUJIELEZA KUHUSU KAULI YA CHATANDA?

Na Joseph Ngilisho|Arushadigital


Chama Cha Mapinduzi (CCM) kimeibua mjadala mpya wa kisiasa baada ya kupita kwa muda uliotolewa na Ofisi ya Msajili wa Vyama vya Siasa wa kukitaka kuwasilisha maelezo kuhusu kauli tata ya Mwenyekiti wa Umoja wa Wanawake wa Tanzania (UWT), Mary Chatanda, bila kuwepo taarifa yoyote ya wazi kuhusu utekelezaji wa agizo hilo.

CCM ililimwa barua yenye maelekezo kuwa  hadi Mei 29, 2026 iwe imewasilisha ufafanuzi rasmi kufuatia kauli ya Chatanda aliyesema kuwa angepewa hata dakika moja ya kuongoza nchi, angeimaliza Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), kauli iliyozua mjadala mkubwa ndani na nje ya uwanja wa siasa.

Kupita kwa tarehe hiyo ya mwisho kumeifanya Ofisi ya Msajili wa Vyama vya Siasa kuwa kitovu cha tahadhari ya wadau wa siasa, huku wananchi na wachambuzi wakisubiri kujua iwapo CCM imewasilisha majibu yake au kama hatua nyingine za kisheria na kiutawala zitachukuliwa.

Katika siku za hivi karibuni, suala hilo limeendelea kujadiliwa kwa mapana kwenye mitandao ya kijamii, ambapo wengi wanahoji ukimya uliopo kutoka kwa chama hicho pamoja na mamlaka husika baada ya muda wa utekelezaji wa agizo kumalizika.

Hadi sasa, Ofisi ya Msajili wa Vyama vya Siasa haijatoa taarifa rasmi kwa umma kuhusu hatua zilizofikiwa, hali inayoongeza hamu ya kujua hatima ya suala hilo ambalo limevuta hisia za wadau wengi wa siasa nchini.

Ends...

Post a Comment

Previous Post Next Post

Contact Form