EWURA YAWAWEZESHA WAHARIRI NA WAANDISHI WA HABARI KUIMARISHA UFUATILIAJI WA SEKTA ZA NISHATI NA MAJI

 EWURA YAWAWEZESHA WAHARIRI NA WAANDISHI WA HABARI KUIMARISHA UFUATILIAJI WA SEKTA ZA NISHATI NA MAJI

Na Joseph Ngilisho-DAR ES SALAAM


Dar es Salaam. Mamlaka ya Udhibiti wa Huduma za Nishati na Maji (EWURA) imeendesha warsha ya tathmini ya kuwajengea uwezo wahariri na waandishi wa habari, ikiwa ni sehemu ya jitihada za kuimarisha uelewa kuhusu majukumu, mipaka ya kisheria na utendaji wa mamlaka hiyo katika kusimamia sekta za nishati na maji nchini.

Warsha hiyo iliyofanyika Februari 27, 2026 katika Ukumbi wa SeaShells Hotel imewakutanisha wahariri na waandishi kutoka vyombo mbalimbali vya habari, ikilenga kupima mafanikio ya mafunzo yaliyotolewa awali na kuweka mikakati mipya ya kuimarisha ushirikiano kati ya EWURA na vyombo vya habari.

Akifungua warsha hiyo kwa niaba ya Mkurugenzi Mkuu wa EWURA, Meneja wa EWURA Kanda ya Mashariki, Lorivii Long’idu, amesema vyombo vya habari vina nafasi muhimu katika kuelimisha umma kuhusu majukumu ya mamlaka hiyo, yakiwemo udhibiti wa bei, utoaji wa leseni na usimamizi wa ubora wa huduma za nishati na maji.

Amesisitiza kuwa kuwajengea uwezo waandishi ni sehemu ya mkakati wa EWURA wa kuhakikisha taarifa zinazowafikia wananchi ni sahihi, zenye uwiano na zinazoakisi hali halisi ya sekta. “Mnapoelewa vizuri tunachokisimamia, mnakuwa daraja sahihi kati ya EWURA na wananchi,” amesema.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa MISA Tanzania, Edwin Soko, amesema warsha hiyo ni mwendelezo wa ushirikiano uliopo kati ya taasisi hizo mbili. Amebainisha kuwa mafunzo yaliyopita yalizaa matokeo chanya ambapo jumla ya habari 103 zilichapishwa katika kipindi cha miezi sita zikihusu shughuli za EWURA.

Ameeleza kuwa warsha za tathmini zinalenga kuibua waandishi mahiri watakaoweza kuandika kwa weledi, kuzingatia maadili ya taaluma na kuchochea uwajibikaji katika sekta za nishati na maji kwa manufaa ya wananchi.

Akiwasilisha mada kuhusu mawasiliano ya taasisi na umma, Meneja wa Kitengo cha Mawasiliano kwa Umma wa EWURA, Wilfred Mwakalosi, amesema uongozi unaowajibika umeendelea kutoa elimu kwa wananchi kuhusu matumizi salama ya gesi majumbani, mafuta na umeme, sambamba na kuhimiza watoa huduma za maji kuwapa wateja taarifa sahihi kuhusu matumizi na huduma zao.

Warsha hiyo imehitimishwa kwa wito kwa wanahabari kuendelea kufanya uchambuzi wa kina, kuandika kwa weledi na kuhakikisha jamii inapata taarifa sahihi zinazochochea uwazi, uwajibikaji na maendeleo endelevu ya Taifa.

Ends..

Post a Comment

0 Comments