By arushadigtal-ARUSHA
ENEO la Stendi ndogo Jijini Arusha limekuwa mwiba mkali na kuibua mvutano wa mara kwa mara baina ya wafanyabiashara wanaojiita wajenzi na halmashauri ya jiji hilo kuhusu umiliki .
Leo mei 22,2025 Baraza la Madiwani limeazimia kubomoa vibanda vyote kwa lengo la kuboresha eneo hilo lenye wafanyabiashara takribani 400 kwa lengo la kuongeza mapato ya Jiji kwa kufikisha Wafanyabiashara 2000.
Akizungumza na Waandishi wa habari ofisini kwake Msitahiki wa Jiji la Arusha Maxmillian Iranqhe amesema serikali inawapenda wafanyabiashara na nia yake ni kuona wanafanya kazi katika mazingira yanayoridhisha na kukuza uchumi wao.
Aidha amebainisha kuwa lengo la kutaka kufanya maboresho katika eneo hilo, ni kutaka wafanyabiashara kufikia 2000 kutoka idadi ya sasa iliyopo ambayo ni wafanyabiashara 400.
Amesema kuwa sio busara kwa wafanyabiashara hao kuwa na mawazo hasi juu ya serikali, kwani kazi ya serikali ni kuhakikisha mapato yanaongezeka ikiendana na maboresho ya sehemu ya biashara.
"Hili ni azimio la Baraza la Madiwani, na lazima lifanyiwe kazi, hatuna nia mbaya bali tunataka kuona wafanyabiashara wakiongezeka ili kukuza mapato yetu" ameeleza Iranqhe.
Hivi karibuni Wafanyabiashara na wamiliki wa maduka hayo waliandama kwa mkuu wa wilaya ya Arusha Joseph Mkude,kulalamikia halmashauri hiyo kuyafunga maduka yao kwa makomeo kwa madai ya wafanyabiashara hao kushindwa kulipa kodi ya maduka wanazodaiwa na jiji hilo .
Hata hivyo dc Mkude alisitisha kufunga maduka hayo na kutaka halmashauri kwenda kufungua ili Wafanyabiashara watafute pesa waweze kulipa madeni yanayowakabili ya halmashauri ya jiji la Arusha yanayofikia bilioni 5.
Pia aliwaeleza kuwa hakuna mpango ya kuvunja maduka hayo kwa sasa na kama utakuwepo watajulishwa.
Sambamba na hayo amewataka wananchi kuwa wavumilivu katika kipindi hiki cha mvua na baada ya hapo ukarabati wa barabara za ndani utaendelea kufanyika kama utaratibu ulivyowekwa hapo awali.
"Vifaa vipo kinachosubiriwa ni kipindi hiki cha mvua kupita ili kazi iendelee" amebainisha Iranqhe.
Mmoja wa wafanya biashara katika eneo la stendi ndogo (hakutaka jina litajwe) amesema suala la maboresho kama lilivyotajwa ni uonevu na nia ya kutaka kurudisha nyuma hatua zao za maendeleo.
"Sikubaliani na mambo ya maboresho, wakiamua wafanye wanavyotaka kwa sababu wana mamlaka, lakini kwa upande wangu hata wafanyabiashara wenzangu hatujawahi kuililia serikali kutuboreshea mazingira yetu ya kazi, kwa miaka yote hiyo tumekuwa tukifanya kazi zetu kwa utulivu lakini sasa naona wanataka kutuvuruga"amesema.
0 Comments